Kwaya hiyo imetembelea kituo hicho Julai 2, 2020, kwa kuimba nyimbo mbalimbali zenye faraja kwa watoto hao wakiwamo weye ualbino, na kutoa msaada wa vyakula, nguo, pamoja na viatu.
Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada huo, Mwenyekiti wa Kwaya ya AICT Shinyanga Kambira Mtebe, amesema wapo katika shamrashamra za maadhimisho ya miaka 43 tangu kuanzishwa kwa kwaya hiyo, ambayo ilianzishwa mwaka 1977, wameamua kutoa msaada kwa watoto hao wenye uhitaji ili wapate pia baraka kwa Mungu.
Amesema watoto hao wenye ulemavu mbalimbali wakiwamo wenye Ualbino, wanahitaji kupewa misaada ya vitu mbalimbali kutoka kwa wadau, ili kuendelea kuwafariji na kujiona kama wapo na wazazi wao, na ndiyo maana wao kama Kwaya wakaona katika kuadhimisha miaka hiyo 43 tangu kuanzishwa kwake watoe msaada huo.
“Kwaya yetu hii ya AICT Shinyanga, tunaadhimisha miaka 43 tangu kuanzishwa kwake mwaka 1977, ambapo maadhimisho haya tumeanza tangu Julai Mosi na tutahitimisha siku ya Julai 5 mwaka huu, na tumefanya huduma mbalimbali yakiwamo maombezi, pamoja na kutoa msaada kwa watoto hawa katika kituo cha Buhangija,”amesema Mtebe.
“Vitu ambavyo tumetoa ni Mbuzi mmoja, Sukari, Mchele, Mafuta ya kupikia,Unga wa mahindi, Juice, Biskuti, Pipi, Maji ya kunywa, Sabuni za kufuria, kuongea, Nguo pamoja na Viatu, Thamani ya vitu vyote ni Shilingi 700,000/=, lengo likiwa ni kuwafariji watoto hawa pamoja na Kwaya yetu ipate baraka,” ameongeza.
Naye mtoto Kwandu Masunga akitoa shukrani kwa niaba ya wenzake, wameishukuru Kwaya hiyo kwa kutoa huduma ya nyimbo na msaada wa vitu mbalimbali vikiwamo chakula na nguo, na kuomba wadau wengine wajitokeze kwenda kuwafariji.
Kwa upande wake mwalimu Mkuu wa shule ya Msingi Buhangija Selemani Kipanya, ambaye ndiye mlezi wa kituo hicho, amesema kwa sasa kuna jumla ya watoto wenye ulemavu mbalimbali wapo 230 kati yao wasioona 26, Viziwi 74, pamoja na wenye ulbino 140.
TAZAMA MATUKIO KATIKA PICHA HAPA CHINI