Header Ads Widget

CHANJO YA ROTA ILIVYOOKOA VIFO VYA WATOTO CHINI YA MIAKA MITANO




Mratibu wa chanjo mkoa wa Shinyanga Timothy Sosoma

Na Kareny Masasy,

MPANGO  wa chanjo hapa nchini ulianza mwaka  1975  kukiwa na chanjo 3 tu hadi kufikia   mwaka  1980 chanjo zimekuwa zikiongezeka  hadi kufikia  chanjo 14 za aina tofauti tofauti zinazotolewa kwa binadamu mpaka sasa.

Chanjo ya Rotavirus   inayotolewa kwenye mwili wa binadamu imelenga  hasa watoto chini ya umri wa miaka mitano  ambayo imeelezwa na wataalamu  ni kinga dhidi ya  ugonjwa hatari wa kuhara.

Katika kitabu cha programu jumuishi ya Taifa  ya Malezi,Makuzi na Maendeleo ya  Awali ya Mtoto  PJT-MMMAM  2021/2022-/2025/2026  kinaeleza  ugonjwa wa kuhara huathiri  asilimia 12  ya watoto chini ya umri wa miaka mitano.

Pia   kunachangia  hadi asilimia 50  ya utapiamlo kwa watoto na kusababisha  watoto kutofikia  hatua  zao timilifu za ukuaji.

Kitabu hicho kinaeleza hatari ya magonjwa ya maambukizi   miongoni mwa watoto  imeongezeka  kwa  kaya chache  huku asilimia 2.7 ya watu kwenye kaya wameripotiwa kutumia sabuni  wakati wa kunawa mikono angalau mara mbili kwa siku.

Mkazi wa kijiji cha Ntobo halmashauri ya Msalala  Pendo Robert  anasema  mtoto wake ana miezi nane  amepata chanjo ya Rotavirus kwa njia ya matone  ambayo inamzuia kuhara  elimu amepewa na wataalamu wa afya na  hajapata tatizo lolote.

 “Tunapata elimu ya chanjo   tukipeleka watoto kliniki na tunaelezwa tuhamasishane  pia kuna matangazo huwa  yanapita mitaani  yanaeleza  nakutaja  watoto umri gani wanapata chanjo”anasema  Robert.

Gloria Shija mkazi wa kijiji cha Ntobo  mwenye mtoto wa miaka miwili anasema amempatia chanjo ya kuzuia kuhara  na hajawahi kupata ugonjwa  wa kuharisha mpaka kuishiwa maji.

Mkazi wa kijiji cha Ntobo Samson John anasema   ipo elimu potofu  baadhi ya wazazi wamekuwa  wakidanganyana mtoto atakuwa mdumavu lakini wengi wameanza kuelewa tofauti na zamani.

Mratibu wa elimu ya afya  kwa umma kutoka halmashauri ya Msalala  Peter Ngazo   anasema  mtoto akianza kuharisha  ataishiwa maji  sababu  atakwenda   haja zaidi ya mara tatu kwa siku.

“Dalili ni kuharisha ni  kichefu chefu, atatapika atapata homa na tumbo kujaa gesi au  kuhisi  tumbo  kuchoma choma ,kuuma na kupoteza hamu ya kula  matokeo yake kupoteza maji  lakini akipewa chanjo  vitu hivyo ataviepuka”anasema  Ngazo.

Ngazo anasema upo uhusiano mkubwa kati ya  chanjo na lishe   kwani  atakapo anza mtoto kuharisha  kama hana lishe nzuri uwezekano wa kupata utapiamlo ni mkubwa sababu vitu vinavyomkinga mwilini havitakuwepo nakumfanya kudhoofika au kupoteza maisha.

Ngazo anasema maandalizi ya baadhi ya wazazi kuwapatia watoto chakula wengine hawanawi  mikono  na wanafuga kucha  ikiwa kirusi  kinatoka kwenye kinyesi na kupitia kwenye mikono na mdomoni.

Ngazo anasema   baadhi ya  wazazi wamekuwa wakinyonyesha    wakati mwingine wanashika titi bila kunawa nakumfanya mtoto kuanza kuharisha.

“Mtoto akifikisha umri wa miezi sita anaanza kupewa chakula cha ziada na kadri akiendelea kukua anafundishwa kula mwenyewe hali ya usafi inahitajika  zaidi  ili kumuepusha na magonjwa ya kuhara”ansema Ngazo.

Mratibu wa chanjo  halmashauri ya Msalala  Bazil Kafunja  anasema zipo chanjo zaidi ya tisa ambapo kuna chanjo ya Rotavirus  zinatolewa kwa watoto kwa lengo la kumzuia kuharisha.

Kafunja anasema upo umuhimu wa watoto kupata chanjo umri mdogo mzazi asipofanya hivyo atamuweka mtoto kwenye hatari  kwani wazazi wanashauriwa  wazingatie maelezo ya  wataalamu  wapate chanjo zote ikiwemo chanjo ya  Rotavirus

“Chanjo ni kumkinga mtoto  kwani hawezi kujikinga mwenyewe na  tunapompatia chanjo tunamhakikishia ulinzi wake imara wa kutopata maradhi na kupoteza maisha”anasema Kafunja.

Kafunja anasema   uchafu au kinyesi ni chanzo cha kuhara kwa mtoto kinasababishwa na wazazi  ambao hawazingatii suala la usafi wa mwili na mazingira wanayoishi  ndiyo maana analindwa kwa chanjo akiwa bado umri mdogo wa kutojitambua.

Kafunja anasema  mtoto asipopatiwa chanjo  akiwa  na miezi sita na mwaka mmoja  na nusu anaweza kupewa chanjo zingine   lakini siyo ya Rotavirus kwani zenyewe zinahitajika mtoto apatiwe kuanzia   umri wa  wiki sita hadi wiki 14.  

Kafunja anasema hata takwimu za magonjwa ya kuhara kwa watoto zimepungua ambapo utolewaji wa chanjo ya Rotavirus kwa watoto chini ya umri wa miaka mitano katika kampeni iliyoisha mwezi Juni   halmashauri ya  Msalala imefikia asilimia 138.

Mratibu wa chanjo mkoa wa Shinyanga  Timothy Sosoma anasema  chanjo ya Rotavirus imeweza kuwafikia watoto  wenye umri chini ya miaka mitano 39512  sawa na asilimia 109 hadi kufikia Juni 2023.

Sosoma anasema malengo ya  upataji wa chanjo hiyo  kwa watoto ilikuwa kuwafikia watoto  39192  hivyo walihamasisha  na kuvuka lengo.

Daktari bingwa  wa watoto kutoka hospitali ya rufaa ya mkoa wa Shinyanga Mwita Ngutunyi anasema   watoto hawaugui sana kuharisha mpaka kulazwa wamekuwa wakiugua kawaida na kuishia kutibiwa katika ngazi za  Zahanati au vituo vya afya.

 Ofisa program wa chanjo  kutoka wizara ya afya  Lotalis  Gadau anasema lengo la kutoa chanjo ni kujikinga na Maradhi  mbalimbali yanayoambukizwa kwa njia ya hewa kwa watoto chini ya umri wa miaka mitano.

Gadau anasema chanjo ya Rotavirus inazuia kuhara kukali  ilianzishwa mwaka 2013 baada ya mwaka  2012 kesi nyingi za watoto chini ya miaka mitano   zilikuwa  za kuhara  baada ya kufanya utafiti mdogo.

 “Mtoto alikuwa akipatwa na tatizo la kuhara kukali alikuwa anaishiwa maji hadi kufikia hatua ya kupoteza maisha lakini sasa kesi hizo hakipo tena”anasema Gadau.

Gadau anasema mtoto anajisadia kwenye poti badala ya kupeleka chooni kinatupwa shambani wakati mwingine mtoto kuchezea mdoli anakuwa akiuweka mdomoni  huenda mdoli huo ukawa mchafu mtoto kupelekea kuharisha.

Gadau anasema hapa nchini watoto hupata chanjo ya Rotavirus kwa awamu tatu  ambapo mwaka 2021 watoto zaidi ya  Millioni 2.3 walipata chanjo na mwaka 2022 watoto Millioni mbili wamepata chanjo.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka Tanzania Demographic  Health Suvey ( TDHS) ya mwaka 2015/2016  inaeleza kuwa asilimia 80  ya kaya  hazina utaratibu  mzuri   wa usafi wa mazingira na utupaji wa kinyesi.

Shirika la afya duniani  (WHO) lilieleza  takribani watoto 450,000 hufariki  kila mwaka duniani kote kutokana na virusi  vya Rota vinavyoishi kwenye kinyesi  cha binadamu kinachosababisha kuhara






Post a Comment

0 Comments