Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) Bi.Mwamini Malemi, akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa 52 wa Baraza Kuu la Wafanyakazi wa NSSF. Bi. Malemi alisisitiza uboreshaji wa huduma bora kwa wanachama, kuendelea kuwajengea uwezo wafanyakazi, kuongeza kasi ya ukuaji wa Mfuko kwa kuifikia sekta binafsi na sekta isiyo rasmi na kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika utendaji kazi.
Pia alisema NSSF itaendelea kusimamia maono ya Serikali ya awamu ya sita chini ya Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhakikisha kuwa Watanzania waliopo katika sekta binafsi na sekta isiyo rasmi wanasajiliwa na Mfuko, waajiri kuwasilisha michango stahiki ya wafanyakazi wao kwa wakati.
Lengo la mkutano huo ni kupitia Mpango wa mwaka ujao na Bajeti kwa mwaka 2024/25, ikiwa ni ushirikishwaji wa wafanyakazi katika maamuzi ya kiutendaji. Ufunguzi wa mkutano huo umefanyika tarehe 9 Mei 2024 katika Hoteli ya Malaika Jijini Mwanza.
Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Masha Mshomba, akitoa maelezo ya awali kabla ya ufunguzi wa Mkutano wa 52 wa Baraza Kuu la Wafanyakazi uliofanyika jijini Mwanza. Mkutano huo ulifunguliwa na Bi.Mwamini Malemi, ambaye ni Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya NSSF.



