Header Ads Widget

VIONGOZI WA DINI,SERIKALI NA WADAU WAKUTANA KUJADILI CHANGAMOTO MALEZI YA WATOTO







Viongozi wa dini,Serikali na wadau wajadili malezi ya watoto.

https://mail.google.com/mail/u/0/images/cleardot.gif

Salum Maige, Geita.

 MOJA ya vikwazo katika kukabiliana na ukatili dhidi ya watoto hapa nchini ni uelewa mdogo kuhusu malezi chanya na mawasiliano duni miongoni mwa wana familia pamoja na wazazi kutotimiza majukumu yao ya msingi ya malezi.

 Changamoto hizi zimetajwa na baadhi ya wadau wa watoto pamoja na wizara ya maendeleo ya jamii,jinsia wanawake na makundi maalumu nchini Tanzania waliokutana mkoani Geita hivi karibuni kujadili namna bora ya malezi ya watoto kuanzia ngazi ya familia ili kuondokana na mmomonyoko wa maadili katika familia, jamii na taifa kwa ujumla.

 Mwenyekiti wa baraza la CPCT mkoa wa Geita Mchungaji Joshua William amesema,viongozi wa dini wanao wajibu wa kuzikumbusha familia kuepukana na migogro ambayo inachangia kuporomoka maadili.

 “Sisi kama viongozi wa dini tunao wajibu mkubwa sana kusimamia malezi bora ya watoto kuanzi ngazi ya family, kwani ni kweli maadili yanashuka katika familia na hii inachangiwa na wazazi au walezi kuacha majukumu yao”, anasema mchungaji William

 Naye askofu Stephano Saguda wa kanisa la Tanzania Messionary Revival Church(TMRC) amesema, ni kweli maadili ni mabaya sana kwa sasa katika jamii kutokana na utandawazi ambapo hata familia ikiwa na malezi bora bado watoto wanapotoka nje ya familia wanakutana na vikwazo vya malezi duni.

 “Yapo matangazo ya luninga yanachangia pia mmomonyoko wa maadili,unakuta tangazo linaonyesha mtu akiwa amevaa mtupu,mavazi yasiyokuwa na staha,haya matangazo yangezuiliwa yanachochea maadili mabaya”,anasema askofu Saguda.

 Ameongeza kuwa, wazazi ni chanzo cha familia kwa maana hiyo wanatakiwa kuwa makini sana kuwafundisha watoto maadili ya Mungu maana wakifundishwa maadili mazuri hata wakija kuwa wakubwa wanakuwa viongozi wazuri kuanzia kwenye familia zao hata taifa kwa ujumla.

 Christina Gamba kutoka kituo cha huduma za kisheria mkoa wa Geita(GELAC)anasema, malezi  sahihi ya kumtengeneza mtoto ni kuanzia umri wa miaka 0-8, pamoja na wazazi au walezi kuwa majukumu mengi ya uzalishaji mali hawapaswi kusahau majukumu yao ya malezi kwa watoto.

 “Zipo kesi za watoto zinajitokeza kwa jamii na asilimia kubwa zina,watoto wanakatiliwa kwa kupewa adhabu kuzidi umri wao,wengine kubwaka, hii inatokana na maadili kuporomoka kuanzia ngazi ya familia baada tu ya wazazi kushindwa kutimiza majukumu yao ya malezi bora” anasema Gamba.

 Mkuu wa dawati la jinsia na watoto wilaya ya Geita mkaguzi msaidizi wa polisi Christina Katana amesema, kuna nafasi kubwa sana kwa wazazi kuleta maadili mema kwa watoto ,na hivyo wazazi wanapaswa kuchukua nafasi zao za malezi bora ili kuepukana na uharifu unaotokea katika jamii.

 “Dawati la jinsia na watoto tumekuwa tukitoa elimu kuhamasisha wazazi kuwa na malezi bora kwa watoto, jamii inatakiwa kujikita kusimamia maadili ili kuwa na familia bora,na jamii bora ya baadaye”, amesema Katana.

 Mratibu wa mradi wa Mtoto Kwanza kutoka shirika lisilo la kiserikali la NELICO mkoani Geita Sophia Njete amebainisha kuwa, mradi huo unatekeleza programu jumuishi ya Taifa ya malezi, makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto(PJT-MMMAM) ambapo moja ya majukumu yake ni kuhimiza wazazi na walezi kuwekeza katika malezi bora kwa watoto.

 Amongeza kwa kusema kuwa, uwekezaji mzuri wa malezi ya mtoto ni kuanzia umri wa mwaka 0 hadi 8,  umri ambao ubongo wa mtoto unakuwa kwa asilimia 90.

 “Katika umri huo tukimuandaa mtoto vizuri eneo hili, kuhakikisha kwamba tunatengeneza watoto bora itasaidia kuwa na familia bora, jamii bora na taifa lenye watu sahihi hata wanapokuwa viongozi wa serikali”, amesema  Njete.

 Wakati wadau hao wakikutana kujadili namna bora ya kuimarisha malezi,makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto,jamii imekuwa na mtazamo mseto juu ya namna bora ya kumlinda mtoto mwenye umri wa miaka 0-8.

 Katika mahojiano maalum baadhi ya wakazi wa mkoa wa Geita wamebainisha kuwa, wazazi wamekuwa mbali na watoto,kushindwa kufuatilia mionendo yao hali inayochangia ukatili dhidi ya watoto kwa kukosa malezi bora.

 Mmoja wa wakazi mjini Geita,John Kasenda anasema, ukatili kwa jamii umekidhiri hasa kundi la watoto yakiwemo matukio ya kubakwa,kulawitiwa na kupewa adhabu zenye kuumiza watoto visa vinavyosababisha vizazi vyenye visasi.

 Kwa mujibu wa wizara ya maendeleo ya jamii, jinsia, wanawake na makundi maalum ni kwamba katika kipindi cha kuanzia julai,2023 hadi aprili, 2024 wizara hiyo imeshughulikia  mashauri 5,944 sawa na asilimia 41 yanayohusu familia na matunzo ya watoto na mashauri 3,350 sawa na asilimia 23 yanayohusu watoto waliozaliwa nje ya ndoa.

 Aidha,Katika taarifa ya waziri wa wizara hiyo Dkt.Doroth Gwajibu katika kipindi hicho mashauri 3,411 yalifikishwa kwa maafisa ustawi wa jamii ambapo 1,642 yalipatiwa ufumbuzi na 443 yanaendelea kufanywa kazi na mashauri 1,326 yalipewa rufaa.

 Mashauri hayo yalipewa rufaa kwenda kwenye vyombo mbalimbali vya usuluhishi ikiwemo mahakama mashauri 921 na mabaraza ya kata na jumuiya mashauri 405.

 Dhima kuu ya kongamano hilo ilikuwa ni kuimarisha uwezo wa wazazi au walezi kwenye malezi chanya ya watoto ambapo serikali imeendelea kufanya jitihada mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuelimisha wazazi au walezi na jamii kuhusu  malezi bora ya watoto sambamba na kuhimiza wajibu wa wazazi au walezi katika matunzo ya watoto na familia.

 Ujumbe wa viongoziwa dini kwenye kongamano hilo ni kuwaasa wazazi au walezi kuongeza jitihada za makusudi katika malezi na makuzi bora ya watoto ili kukabiliana na changamoto za uharifu ukiwemo ukatili unaotokea kwenye familia.

 

 



Post a Comment

0 Comments