Header Ads Widget

WATOTO YATIMA WANAHITAJI MISAADA AINA MBALIMBALI ILI KUTIMIZA NDOTO ZAO

 



Na Mutayoba Arbogast, Kagera

NCHINI Tanzania takriban ni asilimia 47 tu ya Watoto wa wako kwenye mwelekeo wa kufikia ukuaji timilifu. Tafsiri ya taarifa hii iliyotolewa na Idara ya Takwimu ya Taifa inafikirishau maana yake ni takriban nusu ya Watoto wa nchini mwetu ndoto zao za kuwa madaktari, wanasiasa, wafanyabiashara mahiri zinaweza zisitimie na hivyo, badala yake kuwa na ongezeko kubwa la watu wazima tegemezi, vibaka na wasio na tija yoyote kitaifa.

  Leo tunuaangazia kundi ambalo lina uwezekano mkubwa kuwa miongoni mwa hawa Watoto walio katika  asilimia 53 ambao wengi wao wanakosa malezi bora kama yanavyoainishwa kwenye Programu Jumuishi ya Taifa ya Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto ya 2021/22 hadi 2025/26 (PJT-MMMAM). Hili ni kundi ambalo watoto, kwa sababu mbalimbali, imebidi walelewe nje ya kaya au familia zanye Baba, mama, kaka dada na ndugu wengine wa karibu kinasaba kwenye familia, kwani hulelewa kwenye vituo maalum kwa ajili hiyo.

  Vituo vya kulelea watoto yatima hapa nchini vinakumbwa na changamoto mbalimbali ikiwemo uhaba wa raslimali fedha katika kuendesha vituo hivyo na kupelekea kutomudu gharama za kutoa chakula chenye ubora na lishe ya kutosha kwa Watoto wanaoishi huko. Aidha, utelekezaji wa watoto wachanga katika mazingira magumu na hatarishi unaofanywa na mabinti na wanawake, unaongeza idadi ya watoto katika vituo hivyo, hata kusababisha ugumu katika kukidhi mahitaji ya vituo.

  Lishe na ulinzi wa mtoto miongoni mwa maeneo matano muhimu yanayotajwa kwenye PJT-MMMAM kuhitajika kwa mtoto ili aweze kukua kufikia utimilifu wake. Maeneo mengine ni afya, elimu na malezi yenye kuitikia mahitaji na hisia za mtoto.

  Mojawapo ya vituo vinavyopitia changamoto mbalimbali ikiwemo uhaba wa fedha katika kuendesha kituo hicho na kuweza kuwahudumia watoto kikamilifu, sawa na au kukaribiana na watoto wanaoishi na familia zao ni kituo cha kulelea watoto yatima kiitwacho UYACHO, kilichoko kata ya Hamugembe, katika manispaa ya Bukoba mkoani Kagera.

  Kituo hicho chenye watoto 302 kinakabiliwa na uhaba mkubwa wa fedha kuweza kuwahudumia watoto hao kwa kile anachoeleza mmiliki na mkurugenzi wa kituo hichò Bi Saada Selemani (90), kuwa ni kupungua mno kwa misaada ya wafadhili na hivyo kuomba kusaidiwa kupaza sauti yake kwa serikali na jamii kuwasaidia watoto hao.

 Kwa mujibu wa PJT-MMMAM, baadhi ya watoto wanaopata changamoto za kutengwa, kufiwa na wazazi wao au kutelekezwa, wako kwenye hatari kubwa sana yana uwezekano kukumbwa na ukosefu wa usalama, lishe duni na ukosefu wa huduma za afya, utoro shuleni na kukosa watu wa karibu kuwasikiliza shida zao, hivyo programu hiyo inasisitiza kwamba mbinu  ya kutumia mifumo iliyopo kwa malezi itumike na hususan kufuata sera na miongozo ya muktadha kama huo.

 

 Mwezi Aprili 2021, waziri mkuu Kassim Majaliwa, alisema kulikuwa na vituo vya kulelea  watoto yatima visivyopungua 140 nchini,  vikiwa na watoto zaidi ya 24,000. Hili ni kundi kubwa linalohitaji huduma zote stahiki kwa Watoto.

 Mmiliki na mkurugenzi wa kituo hicho cha UYACHO, Bi Saada anakumbusha, "Watoto hawa, wanahitaji msaada mkubwa wa serikali na jamii, maana wafadhili waliokuwa wanatusaidia wamefunga misaada yao, wanasema tujitegemee, nami ndio hivyo nimezeeka nguvu zinapungua kuwahudumia".

  Kituo hicho  kilianza kupokea na kuwalea watoto yatima na wale wenye mazingira magumu tangu mwaka 1999, ambapo baadhi ya waliolelewa hapo wamekwisha kujiimarisha kimaisha katika nafasi mbalimbali za kujitegemea na kulitumikia taifa, huku wengine wakiendelea na masomo ya elimu ya awali, msingi na sekondari katika shule za  Hamugembe,Nyanshenye, Istikama, Kabwoba nk za mkoani Kagera.

  Anasema kwa sasa anao watoto 22 walio chini ya miaka 8 ambao wako madarasa ya awali kwenye shule za msingi.

 Akiongea na waandishi habari waliotembelea kituo hicho hivi karibuni, mkurugenzi huyo amewashukuru sana viongozi wa mkoa, manispaa ya Bukoba na jamii kwa jumla, kwa awamu tofauti walivyomshika mkono katika kuhakikisha kituo hicho kinaendelea kuwahudumia watoto , lakini anaomba jitihada hizo ziwe maradufu kwa kuwa misaada ya wafadhili imepungua mno.

 "Watoto hawa ndiwo baba na mama wa kesho, kwa hiyo tunatakiwa kuwalea kwa kuwatimizia mahitaji yao muhimu sawa na watoto wengine, ili wakue kwa utimilifu wao, na hii inahitaji fedha", anasema mkurugenzi huyo.

  "Niliacha kazi katika halmashauri ya mji Bukoba, wakati ule nikiwa nina nguvu, ili niweze kuwahudumia vyema watoto 42 niliokuwa nao wakati ule, huku nikiwa nimepewa na serikali shamba la kulima mazao mbalimbali kama mihogo na viazi kuwalisha watoto, sasa hivi nimezeeka sina nguvu hiyo", anasema Bi Saada kwa tabasamu huku uso wake ukiwa na alama zote za uzee, akikumbuka enzi hizo, miaka ya 2010 wakati mkuu wa mkoa wa Kagera wa wakati huo, Kanali Fabian Massawe, alipomkabidhi  shamba la hekta 20 katika kitongoji cha Katongo, kijiji Mbale,wilayani Missenyi kwa shughuli za kilimo, ambako sasa pia zinajenga nyumba mbili kuweza kuwajamishia baadhi ya watoto.

 


Post a Comment

0 Comments