Header Ads Widget

VITUO VYA KULEA WATOTO MCHANA VYAANZA KUFUATA MIONGOZO


 Mojawapo ya kituo cha kulea watoto mkoani Shinyanga

Na  Kareny  Masasy, Shinyanga

VITUO vya kulea watoto mchana ‘daycare center’ vimeanza kuchukua hatua  ya  matakwa ya sheria,sera na muongozo dhidi ya kumlinda mtoto.

Sheria hizo mojawapo ni sheria ya mtoto namba 21 ya mwaka 2009 iliyofanyiwa maboresho mwaka 2019 na muongozo uliopo juu uendeshaji wa vituo hivyo ili viendane na sifa stahiki za ukuaji timilifu kwa mtoto.

Ofisa ustawi wa jamii  mkoa wa Shinyanga Lyidia Kwesigabo anasema    vituo vya kulea watoto mchana  zaidi ya kumi vilituma maombi ya kusajili na vimepatiwa usajili.

Kwesigabo anasema  wanaendelea kutoa elimu katika vituo  hivyo ikiwa vituo ambavyo  vilibainika kukosa  sifa kabisa viliweza kufungiwa na kutoruhusiwa kuendesha Shughuli yoyote.

Mwenyekiti wa  vituo vya kulea watoto mchana Damary Mollessi anasema  makubaliano yaliyofanyika hakuna kuendesha kituo bila kuwa na usajili  na wazazi waendelee kuviamini vituo vilivyosajiliwa  ili watoto waendelee kupata elimu changamshi.

“Kwani wazazi wamekuwa wakiamini vituo vya kulelea watoto kwa asilimia 100  na sisi wamiliki tujitahidi kufuata miongozo  na sheria zinavyoeleza”anasema Mollessi.

Mollessi  anasema sasa hivi changamoto ya uanzishwaji wa vituo vya kulelea watoto mchana kiholela umeanza kutoweka sababu ya kujisimamia wenyewe kwanza bila kuangalia maslahi ya fedha kutoka kwa wazazi.

“Tunachoshauri kwa wazazi  wasiwapeleke watoto kwenye vituo ambavyo havijasajili kwani kikipata usajili ina maanisha miongozo inafuatwa na mtoto kuwa katika mazingira salama”anasema  Mollessi.

Masunga Joseph  Mmiliki wa kituo cha kulea watoto mchana  anasema  aliamua kusajili kituo  chake mwaka huu ambapo ana watoto wenye umri wa kuanzia miaka miwili hadi minne alianza na watoto watatu sasa ana watoto 87.

  “Tunapenda wazazi nao waelimishwe kuwa mtoto wa miaka miwli hadi mitano akienda kwenye vituo vya kulelea watoto sio kuandika bali ni kuimba na kucheza ilia pate uchangamfu”anasema  Masunga.

Naibu katibu mkuu wizara  ya Maendeleo ya jamii ,jinsia,Wanawake na Makundi Maalum  Amoni  Mpanju  anasema vituo vya kulelea watoto mchana vinatakiwa kufuata muongozo ili watoto wapate makuzi na malezi bora katika ukuaji wao.

“Ili kufikia ukuaji wenye utimilifu watoto wawe kwenye mazingira bora ya kupata elimu changamshi kwa wakati na umri walio nao katika mazingira salama”anasema Mpaju.

Kwa mujibu wa kitabu cha  Proramu  jumuishi  ya Taifa  cha Makuzi,Malezi na Maendeleo ya Awali ya mtoto  PJT-MMMAM  2021/2022-2025/2026 hapa nchini Tanzania watoto wenye umri wa miaka miwili hadi minne hawajafikiwa  na malezi na makuzi yanayostahili kupatiwa katika ukuaji wao ili kufikia hali ya utimilifu.

Baadhi ya wazazi wenye watoto wanaolelewa kwenye vituo Amina Shija na Gerald  Fabian   wanasema wamiliki wanaposajili hata wazazi wanaondoa hofu juu ya mazingira wanayoshinda watoto, upataji wa lishe na  ujifunzaji unakuwa mzuri.


Post a Comment

0 Comments