Header Ads Widget

PROF:SIZA TUMBO AKABIDHI OFISI KWA KATIBU TAWALA MKOA WA SHINYANGA CP. SALUM HAMDUNI

PROF. SIZA TUMBO AKABIDHI OFISI KWA KATIBU TAWALA MKOA WA SHINYANGA CP. SALUM HAMDUNI

Na. Paul Kasembo, SHY RS.

ALIYEKUWA KATIBU Tawala Mkoa wa Shinyanga Prof. Siza D. Tumbo akabidhi ofisi kwa Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga CP. Salum Rashid Hamduni ambaye ameteuliwa hivi karibuni na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan huku akiwaomba watumishi wote, wadau na wananchi wote Mkoa wa Shinyanga kumpatia ushirikiano RAS Hamduni kama ambavyo walikuwa wakimpatia ili aweze kutimiza majukumu yake kikamilifu.

Haya yamesemwa na leo tarehe 22 Agosti, 2024 wakati akikabidhi ofisi kwenye hafla iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano uliopo ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga ambapo viongozi mbalimbali wamehudhuria wakiwemo na Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Anamringi Macha, Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Julius Mtatiro (Wakili).

Wengine ni Mkuu wa Wilaya ya Kishapu Mhe. Joseph Mkude, Mkuu wa Wilaya ya Kahama Mhe. Mboni Mhita, Kamati za Usalama, viongozi wa Chama Cha Mapinduzu, Wakuu wa Taasisi za Serikali na zisizo za Serikali,viongozi wa Kimila, Kamati ya Maridhiano, viongozi wa wachimbaji wa madini, wadau wa maendeleo na watumishi wote.

"Nichukue nafasi hii kuwashukuru nyote kwa ushirikiano wenu mlionipatia wakati wote katika kutekeleza majukumu yangu, na sasa niwaombe rasmi ushirikiano huo huo muendeleze kumpatia RAS CP. Hamduni ili aweze kutekeleza vema wajibu na majukumu yake hapa mkoani Shinyanga," amesema Prof. Siza Tumbo.

Kwa upande wake CP. Hamduni amemshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kumuwezesha Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kumteua kuwa Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga na kwamba amekuja kuwatumikia Wanashinyanga kama Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga na siyo katika nyadhifa nyinginezo huku akiwaomba ushirikiano wakati wote ili aweze kutekeleza majukumu yake.

Kipekee, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Anamringi Macha amempongeza sana Prof. Siza Tumbo kwa kazi nzuri na njema sana aliyoifanya hapa Mkoa wa Shinyanga, amekuwa Mwalimu wakati wote wa utumishi wake kwa watumishi wengine wote akiwemo yeye mwenyewe RC Macha.

Makabidhiano haya yanafanyika kufuatia mabadiliko ya aliyekuwe RAS Shinyanga ambaye amerejeshwa Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine (SUA)

Post a Comment

0 Comments