Header Ads Widget

WATOTO UMRI CHINI YA MIEZI SITA KUWAPATIA VYAKULA MBADALA WA MAZIWA YA MAMA NI HATARI


 Baadhi ya wazazi wapewa elimu juu ya unyonyeshaji watoto Halmashauri Ushetu

 Na Kareny Masasy,

HAPA  nchini Tanzania  tangu mwaka 2016  wiki ya unyonyeshaji  Maziwa ya Mama  Duniani  imekuwa ikiendana na Malengo  ya Maendeleo endelevu   (Sustainable Develepment Goals) yanayojumuisha kiashiria cha unyonyeshaji  watoto maziwa ya mama pekee nakuhakikisha suala la unyonyweshaji linapewa kipaumbele.

Ukosefu   wa elimu sahihi ya unyonyeshaji   kwa  baadhi ya wazazi Halmashauri ya Ushetu wilayani Kahama mkoani Shinyanga  umesababisha kuanza kuwalisha watoto vyakula vya mbadala wa maziwa kabla ya umri wa miezi sita kutimia.

Mkazi wa kijiji cha Iyogo Amina  Mussa anasema  miaka ya nyuma  walikuwa wakinyonyesha mtoto mpaka anafikia umri wa miaka mitatu lakini  wazazi wa wasasa wanadai majukumu yamewaelemea.

“Wazazi wa sasa wanalazimika kuachisha kwa visingizio vingi kwa kueleza  matatizo ili hali asimyonyeshe mtoto na anapo kaa muda mrefu shambani  maziwa anayakamua chini huo nao ni ukatili kwa mtoto”anasema Musa.

Zubeda Julias anasema wazazi wengine wanakoroga uji mwepesi uliochujwa na kunywesha mtoto kwa madai hashibi anaponyonya maziwa ya mama pekee.

Charles Magili anasema wazazi walio bahatika kuwa na mifugo  au fedha wamekuwa wakitumia  njia ya kuwapa maziwa  ya  ng’ombe  nakuwaacha watoto nyumbani kuwa maziwa hayo watakunywa na kushiba.

Ofisa Lishe  wa Halmashauri ya Ushetu Hadija Nasibu  anawashauri wazazi  siku ya unyonyeshaji iliyofanyika kwenye kijiji cha Uyongo nakueleza  upo umuhimu wa kunyonyesha maziwa ya mama  pekee mpaka afikishe umri wa miezi sita.

Nasibu anasema  siku moja alibainika mtoto mwenye mwezi mmoja  aliletwa hospitalini  aliyekuwa akipewa uji matokeo yake tumbo likajaa  na mtoto kulia muda wote  wanapo waambia  wataalamu usimpe  kitu chochote basi  wafuate maelekezo.

“Wastani wa watoto wanne hadi watano kati ya kumi wananyinyeshwa kwa kipindi cha miezi sita  pekee ya mwanzo huku sehemu kubwa ya watoto hupewa maji wakiwa na miezi miwili na wengine kuanzishiwa  maziwa  na kuwachwa kunyonyeshwa tena”anasema  Nasibu.

Nasibu anasema  hali hiyo inasababisha  kuwepo ongezeko la watoto wenye lishe duni hivyo watakuwa wanatoa elimu ya unyonyeshaji  na makundi ya vyakula vya aina mbalimbali   wakati wa mahudhurio ya  kliniki.

“Watafundishwa namna ya kuandaa vyakula kwa mama wanaonyonyesha na wajawazito  pindi watakapo fanya mahudhurio yote ya kliniki”anasema  Nasibu.

Kaimu Mganga Mkuu  wa Halmashauri ya Ushetu  Dk Jenviva  Gabriel anasema wazazi wengi wamekuwa wakiacha  kunyonyesha  watoto  na kukimbilia shambani  kulima au kuvuna  wakati huo mtoto anahitaji kunyonyeshwa kwani maziwa ya mama yanamfanya mtoto kukomaza ubongo wake.

“Ninawataka kuzingatia  suala la unyonyeshaji  kama ambavyo wamekuwa  wakikumbushwa  wawapo kliniki kwani mtoto  asiponyonya  ipasavyo  anakuwa hana uwezo wa kutunza kumbukumbu  na kile atakachokuwa  anafundishwa awapo darasani kukiweka kwenye ubongo wake”anasema Gabriel.

Ofisa lishe mkoa wa  Shinyanga Yusuph Hamis anasema   asilimia 72 ya watoto chini ya umri wa miaka mitano  wanaupungufu  wa damu  ikiwa baadhi ya wazazi wamekuwa hawanyonyeshi kwa utaratibu unaotakiwa maziwa ya mama ambayo yana virutubishi vingi.

Hamis anasema mkoa wa Shinyanga  una asilimia 83 ya watoto wanaonyonya maziwa ya mama kwa kipindi cha miezi sita pekee.

Hamis  anasema   watoto wenye umri wa miezi 0 hadi 23  ni asilimia 99 walioanzishiwa  maziwa ya mama ndani ya saa moja na walioendelea kunyonya  baada ya saa moja  ni asilimia 3.9.

 “Waliondelea kunyonya baada ya mwaka mmoja ni asilimia 78 wazazi wanaelezwa  umuhimu wa kunyonyesha watoto baada ya kuazaliwa na baada ya kufikisha umri wa  mwaka mmoja  ikiwa wataalamu kwenye  vituo vya afya wameendelea kutoa elimu”anasema  Hamis.

Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Watoto kutoka hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Shinyanga  Dk Justina Tizeba anasema  wazazi wamekuwa chanzo cha kuwapatia watoto magonjwa yasiyo ambukizwa hasa upungufu wa damu na udumavu.

“ukosefu wa madini ya vitamin A  utamfanya mtoto kuwa na uoni hafifu au kutokuona kabisa na  ukosefu wa madini chuma  unachangia upungufu wa damu mwilini  na  madini joto unamfanya mtoto kutokukua vizuri hivyo lazima anyonyeshwe vizuri maziwa ya mama ”anasema  DK  Tizeba.

Kwa mujibu wa Taasisi ya chakula na lishe  nchini( TFNC )  inaeleza mnamo mwaka 1990  mkutano wa wataalamu wa lishe ulifanyika  nchini Italia  lengo  kujadili mwelekeo wa kisera kuhusu kuendeleza unyonyeshaji Watoto maziwa ya mama.

Mkutano huo uliohisaniwa na mashirika ya Umoja wa Mataifa ya WHO (Shirika la Afya Duniani) na UNICEF (Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto) Ulifanyika  mwaka 1990

Azimio lililopitishwa na nchi wanachama  kuweka mazingira wezeshi kwa wanawake kuweza kunyonyesha watoto wao maziwa ya mama pekee katika kipindi cha miezi 6 ya mwanzo .

Kwa mujibu wa shirika la Utangazaji  Nchini Uingereza( BBC) limeeleza  kwa takwimu za hivi karibuni za shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto (UNICEF) zinakadiria kuwa unyonyeshaji usio wa kutosha husababisha asilimia 16 ya vifo vya watoto kila mwaka.

Shirika la Afya Duniani (WHO) linahimiza akina mama kuungwa mkono na jamii, familia, na wahudumu wa afya wakati wa kunyonyesha.

 

Post a Comment

0 Comments