Header Ads Widget

RC TABORA PAUL CHACHA AKIWA NA KAMATI YA ULINZI NA USALAMA WATEMBELEA MRADI WA MAJI YA ZIWA VICTORIA IHELELE

RC TABORA PAUL CHACHA AKIWA NA KAMATI YA ULINZI NA USALAMA WATEMBELEA MRADI WA MAJI YA ZIWA VICTORIA IHELELE

Na Marco Maduhu,IHELELE

MKUU wa Mkoa wa Tabora Paul Matiko Chacha, akiwa na kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa huo,wametembea chanzo cha uzalishaji Maji ya Ziwa Victoria Ihelele kilichopo wilayani Misungwi mkoani Mwanza.
Chanzo hicho cha Maji ya Ziwa Victoria kina simamiwa na kuendeshwa na mamlaka ya maji safi na usafi wa mazingira Kahama Shinyanga( KASHWASA)ambapo huyazalisha, na kuyauza kwa jumla kwenye mamlaka za maji,migodi na vyombo vya watoa huduma ya maji ngazi ya jamii, ambayo maji hayo yanafika hadi mkoani Tabora.

Ziara hiyo imefanyika leo Oktoba 16,2024 katika chanzo cha uzalishaji maji Ihelele, kwa kuona namna maji yanavyovunwa kutoka ndani ya Ziwa Victoria,kutibiwa na hadi kumfikia mteja.
Meneja huduma kwa wateja kutoka KASHWASA John Zengo, awali akisoma taarifa kwa ugeni huo,amesema mradi huo wa maji ya Ziwa Victoria ulianzishwa mwaka 2003 na kukamilika 2008, na 2009 ndipo KASHWASA ikaundwa.

Anasema kipindi hicho walikuwa wakizalisha maji na kuyauza kwa jumla kwenye malmaka mbili za maji Kahama na Shinyanga, na walikuwa wakizalisha maji kwa siku Lita milioni 18.
Amesema mradi huo sasa hivi una hudumia mikoa sita ambayo ni Mwanza,Shinyanga,Simiyu, Singida,Geita na Tabora.

Ametaja miji ambayo wanaihudumia maji katika mikoa hiyo kuwa ni Ngudu, Kishapu, Maganzo, Shinyanga Manispaa, Nyan’ghwale, wilaya ya Shinyanga, Isaka, Kahama Manispaa, Kagongwa,Nzega, Igunga,Uyui na Tabora.
"Mradi huu una uwezo wa kuzalisha maji kwa siku Lita milioni 80 na baadhi ya miundombinu inaweza kupanuliwa na kuongeza uwezo wa kuzalisha maji hadi kufikia Lita milioni 120 kwa siku, lakini kulingana na uhitaji sasa hivi tunazalisha Lita milioni 72 kwa siku." amesema John.

Aidha,amesema mamlaka hiyo wapo pia kwenye utekelezaji wa miradi ya maji katika maeneo mbalimbali, na kwamba katika Mkoa wa Tabora wanapeleka maji Kaliua,Urambo na Skonge, na mradi huo utakamilika Oktoba mwakani ukiwa na thamani ya Sh.bilioni 145.7.
Ametaja changamoto kubwa ambazo zinawakabili ni pamoja na uharibifu wa mazingira kwa wananchi kufanya shughuli za kibinadamu kwenye madakio ya maji ya Ziwa Victoria na kusababisha matope kuwa mengi hasa msimu wa mvua, na kuingia gharama kubwa ya kutibu maji na kusababisha uzalishaji wa maji kuwa mdogo.

Ametaja changamoto nyingine ni kutolipwa fedha za bili za maji kwa wakati, na kwamba hadi kufikia Septemba 30 mwaka huu, wanadai Sh.bilioni 15.
Mkurugenzi Mtendaji wa KASHWASA Mhandisi Patrick Nzamba, amesema mradi huo wa maji ya Ziwa Victoria ni mali ya wananchi kwa asilimia 100, na ndiyo maana wamekuwa wakitoa huduma bora ya maji, na kuyasambaza katika maeneo mengi ili kuboresha ustawi wa maisha yao.

Mkuu wa Mkoa wa Tabora Paul Matiko Chacha,pamoja na kupongeza uwekezaji mkubwa wa mradi huo wa maji ya Ziwa Victoria, ameahidi kusaidia ulipwaji wa madeni ya KASHWASA katika Mamlaka za maji Tabora,Igunga na Nzega, kwamba atakaa nao na kuweka mikakati ya kulipa madeni ambayo wanadaiwa ili kutokwamisha uendelevu wa mradi huo.
"Wekeni nguvu kudai madeni ili msikwame kuendelea kuzalisha maji na kuwahumia wananchi, na mimi katika eneo langu la Tabora nitawasaidia kudai madeni yenu,"amesema Chacha.

Nao baadhi ya wajumbe wa kamati ya ulinzi na usalama kutoka Mkoa wa Tabora, wakizungumza katika majadiliano, waliishauri KASHWASA, kwamba katika eneo la utunzaji mazingira ni vyema wakaweka alama kwenye mipaka yao, ili kulinda maeneo yasivamiwe na wananchi, pamoja na kufanya doria za mara kwa mara wakishirikiana pia na Ofisi ya Mkuu wa wilaya.

TAZAMA PICHA HAPA CHINI👇👇
Mkuu wa Mkoa wa Tabora Paul Matiko Chacha akizungumza wakati wa ziara ya Ihelele kwenye chanzo cha uzalishaji maji mradi wa Maji ya Ziwa Victoria.
Mkurugenzi Mtendaji wa KASHWASA Mhandisi Patrick Nzamba akizungumza kwenye ziara hiyo.
Meneja Mawasiliano na Uhusiano KASHWASA Dk. Mwidini Peter akizungumza kwenye ziara hiyo.
Meneja huduma kwa wateja kutoka KASHWASA John Zengo akisoma taarifa.
Mkuu wa Mkoa wa Tabora Paul Matiko Chacha akiwa na kamati ya ulinzi na usalama katika eneo ambalo maji ya Ziwa Victoria huvunwa na kuingizwa kwenye mitambo ya KASHWASA.
Ziara ikiendelea Ihelele.
Mkurungenzi Mtendaji wa KASHWASA Mhandisi Patrick Nzamba akitoa maelezo jinsi wanavyo zalisha maji, kuyatibu,kuyasafirisha hadi kumfikia mteja.


Picha ya pamoja ikipigwa.


Ziara ya Mkuu wa Mkoa wa Tabora na kamati ya ulinzi na usalama katika chanzo cha maji ya Ziwa Vitoria Ihelele.

Post a Comment

0 Comments