Header Ads Widget

DK.NCHIMBI ATOA MAAGIZO KWA WAZIRI WA KILIMO,TAMISEMI


DK.NCHIMBI ATOA MAAGIZO KWA WAZIRI WA KILIMO,TAMISEMI

Na Marco Maduhu,SHINYANGA

KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi CCM Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi, amemuagiza Waziri wa Kilimo Hussein Bashe,kulishughulikia tatizo la upatikanaji wa mbegu za mahindi kwa njia ya mfumo ambapo umekuwa ukisumbua.
Amemuagiza pia Waziri wa TAMISEMI Mohamed Mchengerwa, kuhakikisha kwamba, kabla ya uchaguzi mkuu mwakani kipatikane kituo cha afya cha pili,kati ya Kata mbili za Didia na Lyabukande, ambazo ameomba Mbunge wa Jimbo la Solwa Ahmed Salum kuwepo na vituo vya afya kwenye Kata hizo kutokana na kuwepo kwa wingi wa wananchi.

Dk.Nchimbi ametoa maagizo hayo leo Oktoba 9,2024 wakati akizungumza na wananchi kwenye mkutano wa hadhara katika Mji wa Tinde wilayani Shinyanga, pamoja na kupokea kero 73 ambazo zimewasilishwa na wananchi 32, na kisha kukabidhiwa mkuu wa mkoa wa Shinyanga Anamringi Macha ili azitatue na kumpatia majibu.
Amesema kero ambazo zilitokana kwenye msimu wa kilimo uliopita zifanyiwe kazi,ili msimu wa kilimo ujao zisijitokeze tena, likiwamo tatizo hilo upatikanaji wa mbegu za mahindi kwa njia ya mfumo ambapo umekuwa tatizo.

“Maelekezo ambayo nimeyatoa kwa Mawaziri hawa wawili yafanyiwe kazi ili kuondoa kero kwa wananchi,”amesema Dk.Nchimbi.
Aidha,amewataka pia wananchi wajitokeze kwa wingi kujiandikisha kwenye daftari la wakazi ambalo litaanza Oktoba 11, na kwamba siku ya kupiga kura Novemba 27 wajitokeze kwa wingi kupiga kura, na kuchagua viongozi wazuri watakaowaletea maendeleo.

Pia, amewataka wananchi waendelee kudumisha Amani, na kwamba wasikubali kuivuruga kwa kuyumbishwa na watu wachache.
Katibu wa Itikadi, Siasa, Uenezi na Mafunzo Amos Makalla, amewataka wananchi, waendelee kuwa na Imani na Rais Samia Suluhu Hassan, kwamba ametekeleza miradi mingi ya maendeleo na kila kijiji kimefikiwa.

Mchungaji Peter Msigwa akizungumza kwenye mkutano huo, amesema nchi ipo salama kwenye mikono ya CCM, chini ya Rais Dk.Samia Suluhu Hassan, na kwamba wananchi wasikubali kupotoshwa na wapinzani kuwa watawaletea ukombozi, na wakati nchi ina ukombozi tayari.

Mbunge wa Jimbo la Solwa Ahmed Salum,awali akizungumza kwenye mkutano huo, ameipongeza Serikali chini ya Rais Samia, kwamba tangu aingie kwenye ubunge mwaka 2005 jimbo hilo halijawahi kupokea fedha nyingi kama awamu ya sita.
Amesema alipoingia kwenye ubunge mwaka huo 2005 umeme ulikuwa hauzidi kwenye vijiji 10 na 2020 kulikuwa na umeme vijiji 50, lakini hadi sasa vijiji vyote 126 vina umeme, na kazi iliyobaki ni kusambaza ngazi ya vitongoji.

Amesema kwa upande wa maji kulikuwa na vijiji 32 lakini sasa hivi vijiji vyenye maji ya Ziwa Victoria vipo 72 na vijiji 8 wakandarasi wapo site, na kwamba hadi kufikia 2025 vijiji 107 vitakuwa na maji safi na salama, sawa na asilimia 87.2.
Aidha, amesema Rais Samia ametoa fedha nyingi jimboni humo, na kwamba miradi mingi imetekelezwa, ikiwamo ya sekta ya elimu, afya, maji, barabara na umeme.

Amesema changamoto ambazo bado zipo, ni upatikaji wa vituo vya afya Kata ya Didia na Lyabukande kutokana wingi wa watu, na pia kuna tatizo upatikanaji wa mbegu za mahindi, kwamba wananchi wakifuata mbegu hizo wanakuta mfumo upo chini.

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Anamringi Macha,amesema Rais Samia Suluhu Hassan, ndani ya utawala wake katika mkoa huo, kwamba ameshatoa kiasi cha fedha Sh.bilioni 846 na kutekelezwa miradi mbalimbali ya maendeleo.

TAZAMA PICHA HAPA CHINI👇👇
Katibu Mkuu wa CCM Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi akizungumza kwenye mkutano wa hadhara na wananchi wa Tinde.
Katibu Mkuu wa CCM Balozi Dk.Emmanuel Nchimbi, (kulia) akimpatia kero 73 Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Anamringi Macha, ambazo zimewasilishwa na wananchi ili azitafutie ufumbuzi na kumpatia majibu.
Katibu wa Itikadi, Uenezi na Mafunzo CCM Taifa Amos Makalla akizungumza kwenye mkutano huo.
Katibu wa NEC,Idara ya Mambo ya siasa na uhusiano wa kimataifa Rabia Abdalla akizungumza kwenye mkutano huo.
Mchangaji Peter Msingwa akizungumza kwenye mkutano huo.
Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga Mabala Mlolwa akizungumza kwenye mkutano huo.
Mbunge wa Solwa Ahmed Salum akizungumza kwenye mkutano huo.
Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Anamringi Macha akizungumza kwenye mkutano huo.
Katibu wa CCM Mkoa wa Shinyanga Odilia Batimayo akizungumza kwenye mkutano huo.
Mwenezi wa CCM Mkoa wa Shinyanga Richard Masele akizungumza kwenye mkutano huo.
Viongozi mbalimbali wakiwa meza kuu.
Mkutano wa hadhara ukiendelea.


Post a Comment

0 Comments